Apple kuunda magari yanayojiendesha


Logo ya AppleImage copyrightGETTY IMAGES

Kampuni ya Apple imetangaza mipango yake ya kuunda magari yanayojiendesha. Kampuni hiyo imekiri hayo kwa mara ya kwanza kwenye barua kwa wasimamizi wa uchukuzi Marekani.
Apple imesema inafurahishwa sana na uwezo wa mifumo ya kutumia kompyuta kwenye maeneo mengi, "ikiwemo uchukuzi".
Kampuni hiyo imesema kuna manufaa mengi ambayo yatapatikana kijamii kutoka kwa magari yanayojiendesha.
Kumekuwa na uvumi kwa muda kuhusu mipango ya kampuni hiyo, inayofahamika sana kwa kuunda simu za iPhone na kompyuta, kuunda magari yanayojiendesha.
Hata hivyo, kampuni hiyo ilikuwa haijakiri hadharani mipango hiyo.
Hata hivyo, kampuni ya Ford, ambayo pia ina mipango ya kuunda magari kama hayo, ambayo inadhamiria yataweza kutumiwa barabarani mwaka 2021, ilisema inaendelea na mpango wake ikifahamu kwamba Apple nao wanaunda magari kama hayo.
Tayari Apple imesajili anwani za tovuti mtandaoni ambazo zinahusiana na magari, zikiwemo apple.car na apple.auto.
Google tayari inafanyia majaribio magari yanayojiendesha.
Oktoba, kampuni inayounda magari yanayotumia umeme, Tesla, ilitangaza kwamba magari yake yote sasa yataundwa yakiwa na programu ya kuyawezesha kujiendesha bila kuwa na dereva.
Nchini Uingereza, gari la kujiendesha lilifanyiwa majaribio Milton Keynes majira ya joto, na majaribio zaidi yamepangiwa kufanyika London karibuni.

Previous
Next Post »